MAKUBWA VITA YA FISTULA NCHINI

by Amref Health Africa

Ni ugonjwa unaompa adha ya kiafya na kiheshima na matokeo mazuri yake ni kwamba, mhusika anashindwa kujizuia haja ndogo.

Chanzo cha maradhi hayo ni pale mwanamama anakuwa na uzazi pingamizi, bila ya kuwa na huduma ya haraka kumasaidia.

BOSI CCBRT

Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya CCBRT, Brenda Msangi, anatamka katika Siku ya Kimataifa ya Kutokomeza Fistula ya Uzazi Duniani, kwamba mtu anatakiwa kutafakari, akigeukia alikotoka an aliko sasa, akifikiria namna ya kuendelea na juhudi za kuitokomeza fistula ya uzazi nchini.

Anasema, Umoja wa Mataifa ulianzisha mwongozo wa kutokomeza fistula mwaka 2003, ikiwa ndicho kipindi nacho CCBRT ilianza kutoa matibabu ya fistula.

“Kama mnavyojua fistula inatokea Kwa wingi Afrika, hasa Kusini mwa Jangwa la Sahara na Asia,” anasema Brenda na kufafanua ni miaka mingi sasa mataifa ya magharibi, walishafanikiwa kutokomeza fistula katika jamii zao.

Brenda anasema, ni hatua iliyofikiwa kwa matunda ya juhudi za pamoja na mikakati, jambo linalowezekana katika nchi zinazoendelea katika utokomezaji wa maradhi hayo.

“Kaulimbiu ya mwaka huu inasema fistula ya uzazi ni ukiukwaji wa haki za binadamu tuitokomeze sasa,” anasema Brenda.

Anasema, CCBRT ni moja ya wadau wakuu kwenye harakati za kutokomeza fistula nchini na imekuwa ikitoa mchango mkubwa katika kinga na matibabu.

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, mradi wa mama na mtoto umezuia fistula mpya kutokea mkoani Dar es Salaam, huku katika hospitali ya CCBRT, kukijengwa wodi za uzazi na vyumba vya upasuaji.

Anasema, ni maboresho yanayovifikia vituo vingine vya afya 22 kusaidia utoaji wa vifaa muhimu vya huduma ya uzazi katika hospitali na vituo vya afya 24 na kuimarisha mifumo ya uboreshaji huduma za afya katika hospitali na vituo 23.

Brenda anaeleza kuwa, lingine wanalofanya ni utoaji mafunzo kwa watoa huduma za uzazi na watoto, ili kuimarisha maarifa na stadi zao kikazi, lengo ni kifanikisha huduma bora kwa kinamama, ambao ni moja ya walengwa wakuu katika eneo hilo.

Brenda anasema, CCBRT tangu mwaka 2003 imeishatibu kinamama zaidi ya 7000, katika wastani wa wagonjwa 400 kila mwaka.

Anafafanua kuwa, katika kundi hilo wengi ni jamiii kutoka hali ya chini kiuchumi, asilimia 80 (wastani wa 560) wa elimu isiyovuka ya msingi.

Vivyo hivyo, anasema katika kundi hilo la wagonjwa 560, asilimia 35 katika yao (wastani wa1960)  hawakusoma kabisa.

Anasema, kinamama hao wana uwezo mdogo kifedha unaowafanya wasimudu nauli za kuja na kurudi hospitalini kutoka makwao, gharama za matibabu, malazi na chakula. Wanapatiwa huduma hizo.

KUTOKA UNFPA

“CCBRT pamoja na hospitali washiriki, tunaendelea kutoa matibabu ya fistula kwa kila wanawake wenye tatizo hilo, ambaye anajitokeza bila ya malipo yoyote, ikiwa ni pamoja na nauli ya kuja hospitali na kurudi nyumbani baada ya matibabu,” anaeleza mwakilishi waa  Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu (UNFPA).

Felister Bwana, ni Meneja Programu, Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto, kutoka UNFPA anayesema kuwa kuendelea kuwapo fistula katika jamii, kunamaanisha kuwapo uhaba mkubwa wa baadhi ya huduma.

Bwana, anataja maeneo hayo ni upatikanaji huduma za afya ya uzazi na vikwazo katika mfumo mzima wa afya, changamoto kubwa inayowakabili wanawake na wasichana.

Anasema,  hapo inajumuisha mambo kama umasikini, unyanyasaji wa kijinsia, ukosefu wa elimu, kushindwa kuendelea na masomo, ndoa na mimba za utotoni .

“Kila siku wanawake 800 hupoteza maisha duniani kutokana na matatizo ya ujauzito,” anasema na kuongeza kwamba wapo wengine 100,000 wanaopata tatizo jipya la ugonjwa huo kila mwaka

Bwana anafafanua kuwa fistula ya uzazi ni moja ya majeraha makubwa wapatayo kinamama wakati wa kujifungua, akisema: “Tatizo hili linazuilika na kwa walio wengi wametibiwa kwa njia ya upasuaji.”

Anafafanua kuwa juhudi zimeshafanyika na wakati huo huo, kuna uhitaji mkubwa wa kuwasaidia wahanga wa fistula, kwa takwimu zinaonyesha hali si nzuri.

Bwana anasema, tangu mwaka 2003 UNFPA imekuwa inaongoza kuratibu kampeni kutokomeza fistula duniani, ikishirikiana na wadau wengine.

Anasema, UNFPA inapoadhimisha miaka 50 ya kuzaliwa, inafurahi kusema ilichokianzisha kimewasaidia wanawake na wasichana 105,000 kupata huduma ya upasuaji kutibu fistula, tangu mwaka 2003.

Mwakilishi huyo anataja mwaka huu, ambao unakaribia nusu kuna wanawake na wasichana 10,000 waliokwishafanyiwa kwa msaada wa UNFPA, ni kampeni iliyopo katika nchi 55 za Afrika.

Anaongeza kuwa, kidunia zaidi ya wanawake wasichana 9,000 wamepatiwa mafunzo na ujuzi aina mbalimbali na kupewa mitaji midogo ya kuanzisha biashara baada ya matibabu.

Vilevile, shirika linafanya kazi ya kuwajengea uwezo zaidi ya wahudumu wa afya 4,000 nchini, wamudu kutoa huduma kwa wagonjwa wa fistula.

Nchini Tanzania, anasema UNFPA inashirikiana kwa karibu na baadhi ya wadau kuboresha afya ya uzazi, mama mtoto na vijana, ili kupunguza vifo vya kinamama na watoto na matatizo yatokanayo na uzazi, ikiwamo fistula.

Anataja baadhi ya wadau hao ni Wizara za Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee an Watoto; Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali ya Mitaa (Tamisemi)’ na mashirika mengine yasiyo ya kiserikali, kama CCBRT na Shirika la Afrika  Linaloshugulika na Utafiti wa Tiba – AMREF.

Bwana anasema, UNFPA imeendelea kununua dawa za uzazi wa mpango na dawa zingine zinazotumika kuokoa maisha ya mtoto na mama wakati wa kujifungua, lengo ni kuzuia mimba zisizotarajiwa, zile za utotoni na zinazoendelea kuchangia kutokea fistula.

Kwa mujibu wa ofisa huyo, UNFPA imejipanga kutokomeza fistula ya uzazi ndani ya kipindi cha Malengo Endelevu ya Maendeleo, ifikapo mwaka 2030.

BOSI AMREF

Mkurugenzi Mkazi wa AMREF nchini, Dk Florence Temu, anaitafsiri fistula ya uzazi kuwa ni kiukwaji mkubwa wa haki za binadamu.

Dk Temu anasema, kupitia AMREF yenye umri zaidi ya miaka 60 sasa ikichangia  huduma za afya, mwaka

mwaka 2002 kwa kuungana na wadau wengine, ilichukua hatua za kupigana kutokomeza fistula.

“AMREF tunataka kinamama warudi katika biashara, tumekuwa tukichangia kudumisha masuala ya lishe na kuwalenga vijana walio katika umri wa kuzaa” anasema.

Anaongeza kuwa hivi sasa AMREF imechangia kufungua wodi za wazazi, kuwawezesha mabinti kupata taarifa za uzazi, kuboresha afya zao na lishe kwa jumla .

Dk. Temu anasema tangu mwaka 2002 mpaka sasa, kuna wahudumu zaidi ya 1000 waliowekwa  kutoa huduma hiyo na wamekabidhi vifaa tiba 41 katika ngazi ya wilaya na mkoa.

Anatoa mfano wa wilayani Magu, ambako kuna janga la fistula, waliwasaidia kinamama 50 kurudi katika maisha ya kawaida, ikiwa sehemu ya vita kwa kushirikiana na serikali, kukabili na kukomesha fistula nchini.

TATIBU WA FISTULA

James Chapa, ni daktari wa CCBRT anayetibu ugonjwa wa fistula na Rais wa Chama cha Fistula Tanzania, anasema hivi sasa ni mwaka wa tisa  tangu kuanzishwa chama hicho.

Anasema kuna uwezekano kwa mwanamke kukingwa dhidi ya kuugua fistula na hata kutokomeza kabisa ugonjwa huo, iwapo kunahatua thabiti katika hilo.

Dk. Chapa anasema mwongozo wa kutibu fistula unaandaliwa kwa njia zinazomfanya mgonjwa apate matibabu bora na anafafanua:

“Watu wanaotibu fistula, wanatakiwa wawe na ujuzi mkubwa katika kutoa matibabu na kuhakikisha mama aliyepata fistula hapati tena fistula,” anasema.

Kwa mujibu wa daktari huyo, kila mwaka kuna wagonjwa wapya 3000 wa fistula, lakini wanaofika kupata matibabu ni nusu yao ambao jumla yao ni 1500 .

Anasema madaktari bingwa wa fistula nchini wapo 40 tu, waliopata mafunzo, lakini katika utaalamu wa upasuaji hawafiki 10, idadi ambayo kitaifa ni ndogo sana.

Dk. Chapa anataja mikoa inayoongoza kuwa na fistula ni Rukwa na mikoa ya Kusini mwa nchi, pia anaeleza athari zake kuwa ndoa zimekuwa zinavunjika kila baada ya kuugua fistula.

MGONJWA FISTULA

Rehema Emmanuel, anayepata matibabu hospitalini CTBRT, ni mkazi na mzaliwa wa Bunda mkoani Mara, anayesema ndoa yake imevunjika baada ya kuugua fistula.

Rehema, mwenye  elimu ya msingi, ni mzaliwa wa mwaka 1977, anayesema alifunga ndoa mwaka 1996 na kufanikiwa kupata mtoto 1998, ndipo akapata mtoto fistula, hali aliyoduimu nayo kwa miaka 20.

Anaongeza kuwa baada ya kuugua fistula, alianza kupata manyanyaso katika ndoa hadi kuachika na sasa mumewe ameoa mwanamke mwingine.

Anasema Aprili mwaka huu, alipata wasamaria waliomfikisha CCBRT kupata matibabu na sasa anaendelea vizuri akiwa na matumaini ya kupona .

Wito wake, ni kuwataka kinamama wanaokutwa na hali hiyo, wasiogope kujitokeza kuchuguzwa afya zao na anaongeza kuwa fistula inatibika na sasa anaendelea vizuri kiafya.

Article first published on https://www.ippmedia.com/sw/makala/makubwa-vita-ya-fistula-nchini

You may also like

Leave a Comment

* By using this form you agree with the storage and handling of your data by this website.

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.

This website uses cookies to improve your experience. We'll assume you're ok with this, but you can opt-out if you wish. Accept Read More